Tibazetu Afrika

Blog hii inahusu tiba za asili juu ya magonjwa mbalimbali ya kimwili na kiroho.Habari,burudani na mambo yote yanayoizunguka jamii.

Contact us

+255 657 739713
Whatsapp/call and sms

Email
Tibazetutz@gmail.com

Watembeleaji

Search

Jumapili, 25 Septemba 2016

TAHAJUDI -1



Neno tahajudi limetokana na neno la kiingereza linaloitwa meditation' likiwa na maana ya kufikiri kwa uzingativu au kwa kujali. Neno meditation, nalo limetokana na neno la kilatini linaloitwa meditatio' likiwa na maana ya mazoezi ya mwili na akili.
Asili ya tahajudi ni dini za mashariki. Ilianzia huko Asia zaidi ya miaka 5,000 iliyopita. Kwa sasa tahajudi hufanywa zaidi huko magharibi (Ulaya na Marekani).
Tahajudi ya miaka hii (ya wakati huu), inazungumzia zaidi tahajudi ya kiyoga ambayo asili yake ni huko India.
Kwa ujumla, tahajudi inaelezwa kama njia za uzingativu katika jambo ambalo mawazo yamelinuia. Lakini pia inaweza kuelezwa kama ifuatavyo:
· Ni hali ya uzingativu na utulivu katika hali halisi ya wakati wa sasa hivi.
· Ni ile hali wakati mawazo yanapokuwa yameyeyushwa na kufikia mahali ambapo hakuna fikra yenye kuingia tena.
· Ni ile hali ambayo, uzingativu, kwa makusudi kabisa umeachwa kuelekea kwenye nguvu kubwa zaidi ( Mungu? Nguvu kuu? ).
· Ni ile hali ya kuweka mawazo na uzingativu katika kitu kimoja, mfano- sanamu ya kidini, pumzi au neno fulani unalotamka (mantra).
· Wengine wanaielezea tahajudi kwamba, ni sala za usiku wa manane.
                             TAHAJUDI NA DINI
Kila dini ina aina yake ya uzingativu, ingawa ukiutazama kwa undani utagundua kwamba ni tahajudi halisi.
Dini ya kikristo wanatumia rozari, hii huwasaidia kujenga uzingativu. Waislamu wanatumia tasbihi ambayo huwasaidia kujenga uzingativu, lakini pia huwa wanakuwa na sala za usiku wa manane (tahajudi). Wabudha huwa wanafanya tahajudi kila siku kwani ndiyo nguzo yao kuu. Wabahai, hufanya tahajudi kila baada ya sala.
                    FAIDA ZA TAHAJUDI
Ili uweze kutambua faida za tahajudi, ni muhimu kuifanya kila siku, ikiwezekana asubuhi na jioni. Tahajudi ina faida nyingi sana, faida hizi utaziona tu kama utafanya tahajudi kila siku. Hivyo, tahajudi inahitaji nguvu kubwa sana ya kujituma (wheel power). Ina faida kubwa sana, hivyo ni vizuri ukajenga mazoea ya kuifanya kila siku. Nakushauri, kama huwezi kufanya tahajudi, basi ni afadhali ujifunze upendo ingawa, ni rahisi mara kumi kufanya tahajudi kuliko kuwa na upendo. baadhi ya faida hizo ni kama ifuatavyo:
1. Husaidia kuongeza ubora wetu kiakili, kimwili pamoja na uwezo wetu kwa ujumla. Husaidia kuuburudisha mwili, pia husaidia kupumzisha akili na mwili.
2. Husaidia kujenga uzingativu na kukuwezesha kumudu kupata suluhu ya matatizo kirahisi.
3. Husaidia kuratibu msukumo wa damu pamoja na usafirishwaji wa damu mwilini.
4. Husaidia pumzi pamoja na kurahisisha usagwaji wa chakula mwilini.
5. Husaidia kuimarisha mfumo wa kinga mwilini.
6. Husaidia kuleta furaha ya nafsi.
7. Husaidia kuimarisha nguvu yako ya machale pamoja na nguvu zako za ziada.
8. Husaidia kutibu matatizo mengi ya kisaikolojia kwani hubadili hali ya mfumo wa fahamu na mawazo (endapo itafanywa kila siku).
9. tahajudi pia inaweza kutumika kuomba kitu unachohitaji, kama vile kazi au mahitaji mbalimbali, ingawa inashauriwa uwe mwangalifu badala ya kufanya kazi unaweza ukawa mtegemezi wa tahajudi. Mfano, unaweza ukatumia tahajudi kuomba shilingi laki moja na ukapata bila kufanya kazi yoyote au kwa kufanya kazi kidogo sana ambayo hailingani na malipo ya laki moja.
JE TAHAJUDI HULETA UTAJIRI
Ni swali gumu kwa sababu, utajiri ni dhana pana sana, inategemea tu unazungumzia utajiri upi, wa kitu gani na wapi. Hata ule utajiri wa kimazoea, nao bado ni mgumu kuuelezea. Mfano, tajiri wa kijijini, akihamia mjini anaonekana ni mtu wa kawaida kabisa kwani kuna matajiri wengi sana wanaomzidi.
Lakini, swali la kujiuliza ni hili, unataka utajiri ili iweje au upate nini? Kama unataka utajiri ili uwe maarufu kwa kuandikwa na magazeti, ukweli ni kwamba, kuna uwezekano mkubwa wa wewe kuandikwa na magazeti ingawa siyo kwa utajiri ila kwa kubaka mtoto. Lakini pia kama unataka utajiri ili ukupe furaha na amani, ukweli utabaki palepale kwamba, hata kama utaupata huo utajiri, furaha au amani haitapatikana kwani utakuwa umevunja kanuni ya maisha kwani hukuja duniani kutafuta utajiri, bali kuishi kwa kufanya kazi unayoipenda sana, inayokupa furaha na amani bila kujali maslahi, heshima au umaarufu kutoka kwenye kazi hiyo. Kwa kuwa, kazi hii unaipenda, utaifanya kwa ufanisi mkubwa sana, na ndipo utajiri utakapokuja. Kanuni ya maisha kuhusu utajiri inaanza na kufanya kazi inayokupa furaha na amani na ndipo utajiri unafuata, haianzi na utajiri na ndipo furaha na amani vipatikane. Kama huamini, wachunguze matajiri unaowafahamu, ambao walipata utajiri ili uwape furaha na amani, utagundua kwamba, hawana furaha wala amani. Kwa upande wa pili wa shilingi, wale matajiri ambao, utajiri wao ulikuja kupitia kwa kufanya kazi inayowapa furaha na amani, utagundua kwamba wana furaha na amani kubwa sana.
Swali lililoulizwa hapo juu linasema, je, tahajudi huleta utajiri? Kama utajiri ni kupata furaha na amani ya nafsi, jibu ni ndiyo. Hii ni kwa sababu, tahajudi hukusaidia au kukufundisha namna bora kabisa ya kupumzisha akili na mwili na hivyo kuwa mtu mwenye furaha na amani. Kumbuka, ukishakuwa mwenye furaha na amani, wewe tayari ni tajiri wa mali pia.